JE HAYA NI MAPENZI!! 71: - UHONDO KITANDANI

Hot

Post Top Ad

https://play.google.com/store/apps/details?id=chumba.cha.wakubwa

Wednesday, February 19, 2020

JE HAYA NI MAPENZI!! 71:





Dorry alitamani kumjua huyo mwanamke, alichukua
ile namba na kuijaribisha kwenye mtandao.
Jina likaja pale, "Sabrina Deo"
Dorry akashtuka, akainuka ili aende kumuonyesha
Sakina ile namba na kitabu.
Kabla Dorry hajafika kwa Sakina ili kumuonyesha ile namba, simu yake ya mkononi ikaita.
Alipoangalia mpigaji akaona ni namba ya Sam, na kuamua kupokea bila wasiwasi wa aina yoyote ile, ila upande wa pili iliongea sauti ya kike.
"Nimesoma mpango wenu humu kwenye simu ya Sam"
Dorry akashtuka na kuogopa, akaona kamavile anataka kushtukiwa, akaikata ile simu.
Mashaka yakamjaa kwenye moyo wake, akajikuta akirudisha vile vitu chumbani kwa Jeff kisha akabeba mkoba wake na kwenda kujigelesha kwa mama wa Jeff ili aondoke.
"Mbona hivyo Dorry, uende wapi muda huu?"
"Nimepigiwa simu sasa hivi na bosi, nimeambiwa nifanye hima niende"
"Ila si bado hali yako haijatengemaa mwanangu?"
"Usijali mama, kama nitapata tatizo lolote nitakutaarifu"
Sakina akaumia sana, kwani alipenda kuwa karibu na binti huyu ili amlee mjukuu wake mwanzo mwisho, ila kwavile aling'ang'ania kuondoka hakuwa na jinsi zaidi ya kumkubalia na kumsindikiza tu.

Sabrina alishangaa kwaninh huyo Dorry amekata simu kwani hata alipoijaribisha ile namba haikupatikana tena.
Akaamua kuijaribisha kwenye simu yake lakini bado hakupatikana. Alitamani kuujua mpango wa Dorry na Sam kwa undani zaidi,
"Huyu Sam akija atanieleza vizuri juu ya ajenda aliyokuwa nayo kwa yule binti"
Kitendo cha yule binti kutokujibu kitu zaidi ya halloo kilimpa mashaka Sabrina, akajikuta amejirundikia mawazo ya kutosha kwenye akili yake.

Dorry alifikishwa stendi na Sakina kisha akapanda daladala na kuondoka.
Ila daladala ilipofika mbele kidogo akapata wazo la kwenda kuongea na Sam kwanza,
"Nitampataje sasa ikiwa tu simu yake kapiga mkewe? Mbona nimeumbuka leo!"
Akaona ni vyema aende ofisini kwa Sam kujaribisha kama atampata.
"Nikimkosa basi, nitajirudisha tu Bagamoyo kwa lazima maana sitakuwa na jinsi"
Alijawa mashaka sana kwenye moyo wake.

Sam akiwa pale ofisini kwake, akataka achukue simu yake ili ampigie mteja wake.
Akajipekua lakini hakuwa na simu,
"Au nimeiacha nyumbani? Itakuwa ni nyumbani tu maana ni muda mrefu sijaishika"
Ikabidi amalizie kazi yake ya mwisho ili awahi nyumbani kwake akachukue simu yake.

Wakati Sam ndio anataka kutoka pale ofisini, akakutana na Dorry mlangoni na kumfanya ashtuke,
"Kheee Dorry nini tatizo toto?"
Dorry akamsalimia kwanza pale na kumwambia shida yake,
"Naomba niongee na wewe kidogo tu"
Sam akasogea pembeni na Dorry akizungumza nae, kisha Dorry akamuhabarisha juu ya kupigiwa simu na mkewe, Sam akasikitika sana,
"Yani huyu Sabrina huyu sijui huwa anamatatizo gani na simu yangu. Yeye ni kuikagua tu mwanzo mwisho anapoikuta. Ila usijali"
"Lazima nijali maana mkeo ni rafiki mkubwa wa mama na anaweza kumueleza chochote kile. Ndiomana nimeaga na kuondoka"
"Huo ni wasiwasi wako tu, mi najua jinsi ya kulitengeneza hili"
Ila kwavile Dorry aling'ang'ania kuondoka ikafanya Sam amruhusu tu.
"Ila mambo yakikaa sawa nitakufata basi maana nahitaji ukae huku huku"
"Sawa hakuna tatizo baba"
Kisha Dorry akaondoka naye Sam akaianza safari ya kurudi nyumbani kwake.

Sam alipofika nyumbani kwake akashangaa kwakuto kumkuta Sabrina pale ndani, akaingia chumbani na kumkuta mtoto kitandani amelala,
"Hivi kweli Sabrina anatoka na kumuacha mtoto ndani peke yake? Mmmh!"
Ikabidi atoke nje na kwenda kumuuliza mlinzi wao pale getini,
"Eti mke wangu yuko wapi?"
"Katoka kidogo, kaniambia atarudi muda sio mrefu"
"Kasema anaenda wapi?"
"Hajaniambia anapoenda"
Sam akarudi ndani huku akitikisa kichwa tu na kujiuliza,
"Au ndio kaenda kwa Sakina? Hivi huyu Sabrina atakuwa na akili kweli jamani? Yani kamuacha mtoto ndani kalala peke yake, hivi huyu mtoto akiamka na kuanza kulia atapata wapi msaada?"
Sam alisikitika sana na kumfanya hata ajutie kidogo kumuoa Sabrina.
"Tatizo ni kumpenda huyu mwanamke laiti kama nisingempenda basi asingeweza kunifanyia haya kabisa."
Akatulia ili ajaribu kumsubiri kidogo.

Muda kidogo Sabrina akaingia ndani huku akijisemea,
"Na nimemkomesha"
Akashtuka baada ya kumuona Sam pale ndani sababu hakumtarajia kwa muda ule, Sam naye akamuuliza kwa mshangao,
"Umemkomesha nani?"
Scrina akakaa kimya huku akiinamisha kichwa chake chini.
Sam akamuangalia na kumuuliza tena,
"Ulikuwa wapi? Na kwanini umemuacha mtoto peke yake humu ndani?"
"Sikuwa mbali, na nilijua wazi sitachelewa"
"Sabrina, kumbuka kuwa huyu mtoto bado mdogo, mambo ya kijinga acha mama. Yani elimu yote ile haijakukomboa mke wangu?"
Sam alikuwa akisikitika tu kisha akamwambia Sabrina amkabidhi simu yake, naye Sabrina akampa ile simu wala Sam hakutaka kumuuliza chochote kwa muda huo kwani alijua wazi kuwa atachelewa kufanya mambo yake tu.
Sam akaondoka pale na kuelekea kwenye kazi yake.

Alifika kazini na moja kwa moja akaingia kwenye ofisi yake.
Muda kidogo akafatwa na mfanyakazi wake,
"Bosi samahani, kuna dada hapo nje ana shida na wewe"
Sam akamuuliza ni nani ila mfanyakazi akadai kwamba hamjui.
Sam akamruhusu kuwa amwambie aingie.
Alipotoka yule mfanyakazi wa Sam ndipo yule dada akaingia.
Sam akashuka kumuona na kumshangaa,
"Kheee nini tatizo Neema! Mbona umekuwa hivyo?"
Neema alikaa kwenye kiti sasa, alikuwa amejifunika khanga karibia na uso na alikuwa ameumia usoni.
Sam akamsogelea Neema pale kwenye kochi la ofisini kwake na kukaa karibu yake ili aweze kumsikiliza,
"Nini mtatizo mama?"
"Mkeo kanifanya hivi Sam"
Sam akashtuka na kushangaa,
"Kivipi?"
Neema akatoa simu yake na kufungua upande wa meseji ambapo Sam aliona jumbe zilizofululiza kana kwamba ni yeye alikuwa akichati nae,
"Uko wapi mrembo?"
"Nipo home tu nimejipumzisha"
"Unaweza kuja mitaa ya karib u na huku kwangu? Tafadhari usiseme hapana, nimekumiss sana mwenzio"
"Poa basi, nipe kama nusu saa nitakuwa huko"
"Umefika wapi sasa mama?"
"Nipo hapa karibu na grocery iliyopo karibu na kwako"
"Sogea sogea hadi hapo kwenye mti mkubwa, nakuja sasa hivi"
"Nipo hapa kwenye mti tayari, mbona sikuoni?"
"Usijali mama, sasa hivi nafika"
Sam aliyasoma hayo mazungumzo huku akitikisa kichwa, hapo ilimuonyesha wazi kuwa Sabrina aliitumia simu yake ile kumlaghai na Neema pia, kisha akamuangalia Neema kwa masikitiko makubwa sana na kumuuliza tena,
"Halafu ilikuwaje"
"Mi nimesimama pale nikamuona kijana mmoja na mkeo, nilipotaka kukimbia yule kijana akanikata mtama kisha nikaanguka chini. Halafu mkeo akamwambia yule kijana kuwa anifundishe adabu. Ndio akanifanya hivi."
Sam akasikitika tena na kumwomba msamaha Neema kwa niaba ya mkewe, kisha akainuka nae na kutoka kwa lengo la kumpeleka hospitali.

Walifika hospitali, na Neema akatibiwa vizuri kabisa sababu Sam alijulikana sana kwenye ile hospitali.
Neema alipomaliziwa matibabu yale, Sam akamchukua na kumrudisha nyumbani kwake kisha akamuaga kwani muda nao ulienda sana.
"Asante Sam, nashukuru kwa kunihudumia"
"Usijali, kesho naweza nikaja kukuona"
Kisha Sam akaondoka pale kwa Neema ili awahi kufika nyumbani kwake.

Sam alikuwa akisikitika tu kwenye gari yake dhidi ya tabia aliyokuwa nayo Sabrina kwa kipindi hiko,
"Mbona kipindi kile wakati meseji za Neema zinaingia kwenye simu yangu na simu alikuwa nayo yeye na hakufanya chochote! Kwanini kipindi hiki amekuwa hivi? Mara ampigie simu Dorry kisa tu kaikuta ile meseje, na mara aanze kumtafuta Neema kwa ugomvi, kwanini Sabrina kawa hivi? Lazima kuna kitu"
Sam aliwaza sana bila ya kupata jibu lolote la maana.

Alipofika nyumbani kwake, alimkuta Sabrina kalala kwenye kochi huku mtoto naye akiwa pembeni anacheza cheza.
Sam  akamshtua Sabrina,
"Hivi kwa mfano mtoto akabilingika hapo na kuanguka utasemaje? Au utamlaumu nani?"
"Hawezi kuanguka bhana nimemshikilia"
"Umemshikilia wakati umesinzia? Sabrina acha masikhara kwa mtoto tafadhari, nampenda sana mwanangu"
Sam akamuinua yule mtoto na kumbeba mikononi na kuanza kucheza cheza naye ingawa alikuwa na mawazo ila alijitahidi kuyapoteza kwa kucheza na mtoto.
Wakati huo Sabrina nae aliendelea kulala pale pale kwenye kochi kitendo ambacho kilimchukiza Sam.
Kwavile alikuwa na hasira tayari, mtoto alipolala akaenda kumlaza chumbani naye akaenda kulala pia na kumuacha Sabrina pale pale sebleni.

Sabrina alishtuka saa kumi ya usiku na kujishangaa kuwa yupo mwenyewe sebleni.
Akasikitika na yeye,
"Yani huyu mwanaume hata kunishtua kuwa nikalale chumbani! Yani yeye kaniacha hapa hapa sebleni? Mbona amekuwa hivi hivi huyu mwanaume jamani?"
Sabrina alisikitika sana dhidi ya hiki  alichokifanya Sam.
Kisha akainuka na kwenda kulala chumbani na yeye.

Kulipokucha Sam akainuka na kujiandaa na kwenda zake ofisini.
Alipokuwa kwenye gari alijisikitikia sana juu ya swala lake zima la kuoa.
"Ndiomana vijana wengi hawaoi, sasa mwanamke wa namna hii ni wa kazi gani? Mwanamke asiye na shukrani. Apate mimba ya mwanaume mwingine nilee mie mimba hadi mtoto, kila kitu nafanya mie ila bado haridhiki anataka kunipandia kichwani kabisa. Lazima nifanye kitu, kumpenda isiwe sababu ya yeye kufanya anavyojisikia. Kwanza kashanitia hasara sana huyu mwanamke na lazima nifanye kitu"
Sam alikuwa akilalamika tu njia nzima.
Aliona kuoa kwake imekuwa kero na karaha badala ya raha alizopata kusikia kwa wengine.

Sabrina nae alichukizwa na kitendo cha Sam kumuacha pale sebleni peke yake.
"Anafikiri kwetu tuna dhiki huyu mwanaume. Kunisomesha kwake sio kwamba nilikuwa mjinga. Nina akili zangu timamu na ninarudi kwetu. Sina dhiki mie."
Sabrina akaanza kujifungasha na mizigo yake ili arudi kwao.
Alipomaliza akampigia simu dereva wa gari za kukodi ili aje amfate.
Na yule dereva hakukawia kufika, kisha Sabrina akatoka na mtoto wake hadi kwenye gari.
Mlinzi wa nyumba ya Sam akamshangaa,
"Vipi mama?"
"Naenda nyumbani"
"Mbona umebeba na mabegi?"
"Kwani umeambiwa nikiwa naenda kwetu nisiende na mabegi?"
Ikabidi mlinzi akae kimya na kumuacha Sabrina aende zake, naye Sabrina akaondoka na mtoto wake.

Dorry akiwa Bagamoyo alikuwa na mawazo sana, alijikuta akimuomba Mungu kwa kila hali kuwa Sabrina asiwe ameelewa vizuri ule ujumbe.
Wakati akiyawaza hayo, wazo lingine likamjia nalo ni kuhusu barua,
"Uwiii barua, ile barua nayo inabidi niichome moto kwani inaweza kuonwa na mtu asiyependa maendeleo yangu kisha ikawa nongwa"
Akaenda ndani ili atoe toka kwenye mkoba wake.
Ila alipekua ule mkoba pasipo uelekeo wa kuipata, akaamua kumwaga kila kitu kitandani ila hakuiona. Akaanza kuvuta kumbukumbu zake dhidi ya mahali alipoiacha ile barua.
Kumbukumbu zikamjia na kumfanya ashike kichwa na kujutia zaidi.
Akakumbuka kuwa kulikuwa na karatasi za vipimo vikionyesha kuwa yeye ni mjamzito na ile barua pamoja na kile kitabu kidogo, vyote aliviacha kitandani kwa Jeff.
"Mungu wangu, hivi mama wa Jeff akiviona nitaficha wapi sura yangu mie? Uwiii hii aibu nitaiweka wapi mie!"
Dorry alikosa raha gafla, huku akiwaza kurudi kwakina Jeff na upande mwingine ukimwambia kuwa atakuwa ameshachelewa.
Dorry alihisi kuchanganyikiwa kwa siku ya leo, alijikuna kichwa kila mara ili kujaribu kuwa sawa.

Sabrina alifika nyumbani kwao na kuingiza mizigo yake ndani, na kumfanya hata mama yake amshangae.
"Weee Sabrina wewe, si umeondoka hapa majuzi tu! Vipi leo umerudi na mabegi?"
"Kwahiyo umenichoka mama?"
"Sio kwamba nimekuchoka, bali nimekuuliza tu"
Ikabidi mama yake amsaidie kuingiza ile mizigo ndani ili apate kumsikia hoja zake.
Sabrina alipoingia ndani kwao hakutaka hata kukaa sana kwani alimuachia mama yake mtoto kisha akamuaga,
"Unaenda wapi sasa?"
"Naenda kwa Sakina nina shida nae sana"
"Shida gani hiyo?"
"Nikirudi nitakwambia mama"
Kisha akaondoka.

Sakina akiwa nyumbani kwake, akaona ni vyema kuangalia usafi ambao Dorry alisema kuwa ameufanya kabla ya kuondoka.
Alipoingia chumbani kwa Jeff akashangaa kuona  karatasi kitandani.
"Kheee ndio usafi gani huu kuacha karatasi kitandani!!"
Akaamua kuzikusanya, ila akashtuka kidogo na kujisemea.
"Huenda zikawa karatasi za maana"
Akakaa pale kitandani ili azipitie kidogo.

Itaendelea



No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

https://play.google.com/store/apps/details?id=chumba.cha.wakubwa