JE HAYA NI MAPENZI!! 51: - UHONDO KITANDANI

Hot

Post Top Ad

https://play.google.com/store/apps/details?id=chumba.cha.wakubwa

Tuesday, February 18, 2020

JE HAYA NI MAPENZI!! 51:






Jeff akajikuta gafla akianza kufoka,
"Inamaana sitakuwa na haki yoyote juu ya mtoto
wangu mwenyewe?"
Muda huo Sam nae alikuwa ameingia pale ndani
kwa Sabrina na kujikuta naye akishangaa kufoka
kwa Jeff.
Sam aliamua kuuliza ili ajue kuwa wanazungumzia mtoto gani,
"Mtoto? Mtoto yupi huyo?"
Sabrina na Jeff wakajikuta wote kwa pamoja wakimuangalia Sam, kisha Sam akawauliza tena,
"Nasikia mnazungumzia mtoto, huyo mtoto ni yupi?"
Jeff akataka kuongea kitu, ila kabla Jeff hajasema chochote Sabrina alianza kuongea huku akihusisha na kumbukumbu za mwanzo za maneno yale aliyowahi kumueleza Sam kuhusu Jeff,
"Huyu Jeff ni mjinga kwakweli, eti anataka kwenda kudai mtoto kwa yule binti wa mwanajeshi aliyempa mimba"
"Sasa ndio afoke? Si aende zake tu"
Kisha Sam akamuangalia Jeff na kumwambia,
"Sipendi umsumbue mke wangu haswa katika hiyo hali aliyokuwa nayo, sitaki umsumbue kabisa. Kama una mambo yako nenda ukafoke huko huko"
Muda huu Jeff alijikuta akiwa na hasira sana ila alitambua wazi kama ataongea chochote basi ataweza kusababisha mambo mengine makubwa zaidi, kwahiyo akajiondokea taratib u tena bila ya kuaga wala kuongea chochote cha ziada.

Ukimya kidogo ukatawala, kisha Sam akauvunja ukimya ule kwa kumuuliza hali Sabrina,
"Unaendeleaje lakini?"
"Naendelea vizuri"
"Ila kila siku mimi nakwambia kuhusu huyu Jeff kuwa hafai kuwa karibu ila wewe unamtetea, si unaona sasa alivyokuwa anafoka hapa utafikiri anaongea na mdogo wake. Tatizo amekuzoea sana"
Sabrina aliamua kutetea zile hoja kidogo kwa Sam,
"Hamna bhana, tatizo Jeff bado mtoto. Akikua ataelewa tu."
"Bado mtoto!! Haya mama, sikubishii"
Ikabidi Sabrina aingize maongezi mengine ili kuepusha mzozo usiokuwa rasmi.

Jeff alijikuta akiwa na mawazo sana huku akilaumu utoto wake,
"Laiti kama ningekuwa mkubwa haya yote yasingetokea. Sijui kwanini mama yangu alichelewa kunizaa jamani. Mbona mimi nampenda sana Sabrina kwanini mapenzi haya yananifanya hivi?"
Jeff alijikuta akinung'unika tu, na ili kupunguza yale mawazo akaona ni vyema kama apate kilevi kidogo ili aweze kuchangamsha akili yake na kupunguza mawazo aliyokuwa nayo.
Kwahiyo akaenda baa na kuanza kuagizia pombe aina ya konyagi ili aweze kulewa kwa haraka zaidi.

Mama wa Sabrina akiwa nyumbani kwake huku akiendelea na shughuli zake zingine, akasikia kuna mtu akimuita, na ile sauti ilikuwa ikitokea nje,
"Joy"
Akajiuliza,
"Ni nani huyo tena ambaye hadi leo ananiita jina langu?"
Akaamua kuacha mambo yake na kutoka nje ili akaangalie, ila hakukuta mtu yeyote na kumfanya azunguke hadi nyuma ya nyumba ila bado hakuona mtu yeyote.
Akaamua kurudi zake ndani, akashangaa kumuona mumewe akiwa pale sebleni.
Joy akashangaa sana na kustaajabu kumbe mumewe ndiye aliyemuita ili kumpima akili tu.
Wakafurahi pale na kuanza kuongelea mambo tofauti tofauti kwani ilikuwa ni muda mrefu kidogo tangu mumewe aondoke na siku hii ya leo ndio alikuwa amerudi.
Joy akaona sasa harusi za wanae zikinukia kabisa kwani waliyekuwa wakimuombea na kumsubiria ndio tayari alishawasili, na kumfanya Joy apatwe na hamasa ya kuwataarifu watoto wake kuwa baba yao amerudi.

Sabrina alimtazama Sam kwa furaha baada ya kupokea simu kuwa baba yake amerudi,
"Sam ndoa yetu tayari, karibia tunafunga"
"Ndio ni kweli, karibia tunafunga. Hata mi nimefurahia ujio wa bamkwe wangu"
Ikawa ni furaha huku mipango ya ndoa yao ikiendelea kupangwa na wao wenyewe kwa taratibu kabisa.

Jeff alirudi kwao akiwa amelewa kiasi hata mama yake akamshangaa mwanae,
"Jeff, kumbe huwa unakunywa pombe mwanangu"
Jeff alikaa kwenye kochi, kisha akamtazama mama yake kwa dakika chache na kuinama kidogo, kisha akainua tena kichwa chake na kumuuliza mama yake,
"Mama, mfano wewe ni mwanaume, kwa bahati nzuri ukampa mimba mwanamke umpendae utafanyaje?"
"Yani wewe Jeff loh, nitafanyaje tena hapo zaidi ya kumuoa huyo mwanamke sababu ushasema nimpendae"
Jeff  akamuangalia tena mama yake na kuendelea kumuuliza,
"Na mfano ukasikia kuwa mwanamke huyo anataka kuolewa na mwanaume mwingine halafu mtoto wako anamkabidhi huyo mwanaume utafanyaje?"
"Maswali gani haya leo Jeff? Au ndio pombe hizo mwanangu"
"Sio pombe mama, nijibu kwanza"
"Mie sitakuwa na tatizo juu ya huyo mwanamke kuolewa, huenda ameniona simfai ingawa itaniuma sana ila tatizo langu litakuwa ni juu ya mwanangu. Hapo lazima  nipambane sababu natakiwa kupata haki ya kuwa na mwanangu kwani mtoto huyo atakuwa ukumbusho pekee kwangu juu ya upendo niliompenda mama yake"
"Kwahiyo mama unanishauri nini?"
"Nakushauri nini kuhusu nini?"
"Mapenzi mama, yanautesa moyo wangu"
"Inamaana kuna mwanamke uliyempa mimba mwanangu? Ni mwanamke gani huyo?"
Jeff alitamani kumueleza kila kitu mama yake, ila ilipomjia ile kauli ya Sabrina kuwa wafanye kuwa siri yao aliamua kukaa kimya,
"Mbona kimya mwanangu? Niambie ili nijue jinsi gani nitakusaidia mwanangu"
"Acha tu mama"
Kisha Jeff akainuka na kuelekea chumbani kwake kupumzika kwanza.

Kesho yake, Sabrina alienda nyumbani kwao kumsalimia baba yake na kuweza kuongea nae mawili matatu juu ya mambo yake ya ndoa.
Alifurahi kumuona tena baba yake, na alikutana na kaka yake nae akiwa na lengo kama lake.
Deo akawaambia watoto wake,
"Naona mlikuwa mkinisubiri kwa hamu maana kila mmoja anaongelea ndoa tu hapa. Ila ni jambo jema na nitasimamia vyema swala hili."
"Ndio baba, tena ukiharakisha itakuwa vizuri zaidi"
"Mie sina tatizo, labda nyie mcheleweshe"
Wakakubaliana na baba yao na kufurahi pamoja.
Wakati wakiendelea na mazungumzo, kuna mgeni alifika pale nyumbani kwakina Sabrina, na wote walimshangaa kwavile sura yake ilikuwa ni ngeni machoni pao.
Sabrina akatoka nje kwenda kumsikiliza.
Akamsogelea na kumsalimia,
"Samahani bibi, tukusaidie nini"
"Nisaidie maji tu mjukuu      wangu, yani hapo utakuwa umenipa msaada mkubwa kupita yote duniani"
Sabrina akaona isiwe tatizo sana akaamua kwenda ndani kumchukulia huyo bibi maji.
Baada ya muda kidogo, Sabrina akatoka na kikombe cha maji na kumkabidhi yule bibi ambaye alikunywa yale maji na kumshukuru sana Sabrina, ila kabla Sabrina hajarudi tena ndani kwao yule bibi akamshika mkono na kumwambia Sabrina,
"Samahani mjukuu wangu, najua hunijui wala sikujui ila nimejisikia kukwambia jambo hili"
Sabrina akamsogelea tena karibu ili aweze kusikia kuwa ni jambo gani ambalo yule bibi anataka kumwambia,
"Niambie tu bibi"
"Ni hivi, katika dunia hii kila jambo hutokea kwasababu fulani na hakuna siri itakayodumu milele"
"Mmh unamaana gani?"
"Sina maana yoyote ile mbaya ila moyo wangu umeona nikwambie hilo kwani ipo siku litakusaidia hapo badae"
Yule bibi akamuaga Sabrina bila ya kujua kuwa amemuacha Sabrina akiwa na mawazo kwa kiasi gani.

Sabrina alirudi ndani kwao huku akiwa amenyong'onyea  mpaka baba yake akaamua kumuuliza kuwa tatizo ni nini,
"Aah hamna tatizo baba"
Kisha akawaaga pale na kuanza safari ya kuelekea nyumbani kwake ili aende akajiwazishe huko.

Akiwa njiani, akapigiwa simu na Sam,
"Uko wapi?"
"Nipo kwenye daladala narudi kwangu"
"Kwanini hukunisubiria nije kukufata?"
Sabrina akawa kimya, Sam akamwambia Sabrina kuwa ashuke na kumtajia Sam alipo kisha yeye atamfata mwenyewe.
Sabrina akafanya kamavile alivyoambiwa na Sam ili kuepuka swala la kumchukiza.
Alishuka na kukaa kwenye kituo huku akimngoja Sam aje kumfata.
Kuna mtu akatokea nyuma yake na kumgusa Sabrina, alipogeuka akakutana macho kwa macho na Francis,
"Khee Francis upo?"
"Nipo ndio, mwanaume pekee mwenye mapenzi ya dhati na wewe Sabrina"
"Saivi nimekuwa Francis, sio Sabrina yule wa zamani kwahiyo maneno yenu hata kidogo hayaingii katika akili yangu"
Francis akamuangalia Sabrina kwa makini huku akitaka kuongea neno lingine, ila muda huo huo Sam nae akawasili eneo lile na kumfata Sabrina pale kituoni alipokuwa amekaa.
Alipofika, akamshika mkono Sabrina na kuondoka nae bila hata ya kumsalimia Francis ambaye aliwaangalia hadi walipoondoka na gari kabisa.

Sam alimpeleka Sabrina moja kwa moja hadi nyumbani kwa Sabrina na kuingia ndani huku akihitaji kujua mushtakabali wa ndoa yao,
"Vipi baba anajua kama wewe ni mjamzito?"
"Hapana, ila kesho twende wote ili nimueleze pia kuhusu ujauzito na ukapange nae kila kitu"
"Yule mzee sina tatizo nae kwakweli, kwavile mambo yake ni kizungu tu. Mungu amlinde mzee wetu, kesho tutaenda pamoja"
Sabrina akakubaliana hivyo na Sam kisha Sam akamuaga na kuondoka kwenda nyumbani kwake.

Sabrina alipokuwa amebaki akapokea simu kutoka kwa Sakina, baada ya salamu, Sakina akaanza kumpa malalamiko yake aliyonayo kuhusu mtoto wake Jeff,
" Hebu niambie ukweli Sabrina, huko kuna mwanamke yeyote Jeff kampa mimba?"
Sabrina akafikiria jibu la kumpa Sakina, akahusisha na maelezo aliyowahi kumwambia Sam kuhusu Jeff, akaamua kumwambia Sakina kwa mtindo huo kuwa Jeff kuna binti wa mwanajeshi ndiye aliyempa mimba,
"Yani huyu mtoto wangu anamakubwa kwakweli, kumbe ni kweli? Nilitaka tu kuhakikisha"
"Ndio hivyo dada"
"Tena kesho nataka anipeleke huko kwao na huyo binti ili nikajue mbichi na mbivu"
"Dada mi nakushauri hayo mambo muachie tu Jeff mwenyewe, hata mimi yalishanishinda hapa"
"Kwakweli Sabrina, siwezi kuangalia upuuzi anaofanya Jeff kila siku huku, lazima nifatilie"
Sakina akakata ile simu na kumfanya Sabrina nae apatwe na mawazo tena kwa kiasi fulani kwani hakutegemea kama Sakina atahitaji kuingilia kati swala hilo.

Sabrina aliamua kwenda kulala, ila kabla hajalala alipigiwa simu na Jeff,
"Mamdogo umemwambia nini mama?"
"Sikuwa na la  kufanya Jeff ikabidi tu nimdanganye"
"Sawa umemdanganya, sasa mi kesho nitampeleka wapi kumwonyesha? Maana mama amekazania kuwa nimpeleke kwa huyo mwanamke"
"Hapo utajijua mwenyewe utakachofanya ila mimi tu usinihusishe juu ya hilo"
"Mmmh mi nikishindwa namleta kwako"
Simu ile ikakatika na kumfanya Sabrina ajilalamishe peke yake,
"Toto halina akili kabisa hili, sijui hata limetokea wapi"
Sabrina alilala ila huku akiwa na hasira kiasi.
Wakati amelala, taswira ya yule bibi ambaye alienda muda wa mchana pale kwao ilimjia usoni tena na maneno yale yale yakajirudia na kumfanya Sabrina ashtuke na kuwa na mawazo mengi mengi huku akiendelea kujiuliza kuwa yule bibi alikuwa na maana gani ila hakupata jibu hadi panakucha.

Siku hii Sakina alimkazania mwanae ili akamuonyeshe kila kitu kilichojificha,
"Kwanza kabisa nataka unionyeshe huyo binti uliyempa mimba, nipeleke kwao nipajue hata kama wazazi wake ni wakali  vipi wee nipeleke tu. Sipendi kukuona ukichanganyikiwa kwa mambo ambayo hata mimi mama yako naweza kuyashughulikia. Napenda kuona ukiwa na furaha tu muda wote"
Jeff hakujua ni uongo gani amwambie mama yake ili amridhishe, aliona mama yake kutaka kujua kila kitu kwa hali na mali.

Sam alimfata Sabrina, kisha wote kwa pamoja wakaondoka na kuelekea nyumbani kwa wakina Sabrina ili kuweza kujadiliana kuhusu mipango ya ndoa na kumwambia Deo kuhusu ujauzito wa Sabrina.
Sam akamueleza baba mkwe wake,
"Napenda ndoa yangu na Sabrina iwe wiki ijayo kwavile nahitaji mtoto wetu azaliwe ndani ya ndoa"
Deo akafurahi, ila kabla hajasema jambo lolote wakamuona Jeff na Sakina wakiwa pamoja pale nyumbani kwa wakina Sabrina, ambapo Jeff akasema,
"Siwezi kabisa kukubaliana na jambo hili"
Wote waligeuka na kumuangalia.

Itaendelea



No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

https://play.google.com/store/apps/details?id=chumba.cha.wakubwa